Main Article Content

Majuto ni Mjukuu: Uchunguzi wa Mhusika Ngoma katika Riwaya ya Ua la Faraja


Adria Fuluge

Abstract

Maisha ya mtu ni hadithi inayopaswa kusimuliwa ili kutoa mafunzo kwa jamii kuhusu mapito ya mhusika. Hii inatokana na ukweli  kwamba kila mtu katika jamii ana mambo mazuri na/au mabaya ya kusimulia yanayohusu mapito ya maisha yake. Yapo masimulizi  yanayofurahisha kutokana na matendo ya mhusika na mengine husikitisha kiasi cha kumfanya mhusika kuyajutia maisha yake kutokana  na kufanya au kutofanya jambo fulani. Kwa msingi huo, makala hii ililenga kuchunguza methali inayosema “majuto ni mjukuu” kwa  kuchunguza maisha ya mhusika Ngoma katika riwaya ya Ua la Faraja (2004). Mhusika huyu ameteuliwa kama kiwakilishi cha wahusika  wengi ambao katika maisha yao, walifanya na/au hawakufanya mambo fulani ambapo kutokana na kufanya na/au kutokufanya kwao,  kulisababisha majuto katika maisha yao. Pia, riwaya hii imeteuliwa kama sampuli ya riwaya mbalimbali zenye wahusika wenye sifa kama  za mhusika Ngoma. Data zilitokana na uchambuzi wa riwaya ya Ua la Faraja. Vilevile, Nadharia ya Uhalisia ilitumika kama mwongozo  katika ukusanyaji wa data, uchambuzi na uwasilishaji wa matokeo ya utafiti wa makala hii. Matokeo yanaonesha kwamba ziko sababu kuu  nne zilizosababisha Ngoma ayajutie maisha yake. Sababu hizo ni kukosa uaminifu katika ndoa, kuitelekeza familia yake, kuendekeza  anasa, na kutowajali ndugu zake. 


Journal Identifiers


eISSN: 2958-4914