Main Article Content

Kufanana na Kutofautiana kwa Msamiati katika Lahaja za Lugha ya Kihaya: Mifano kutoka Kihamba na Kiziba


Editha Adolph

Abstract

Makala hii inafafanua dhana za kufanana na kutofautiana kwa msamiati wa lahaja ya Kihamba na Kiziba katika lugha ya Kihaya. Vipengele vinavyohusika katika kuchunguza kufanana na kutofautiana huko ni vipengele vya tahajia na matamshi.  Lengo la ulinganishi na  ulinganuzi huo ni kubainisha ikiwa kuna ufanano na utofauti wa kimsamiati unaojitokeza katika  lahaja hizi mbili za lugha ya Kihaya yaani  Kihamba na Kiziba.  Kwa mujibu wa makala hii, eneo hili halijapewa aula na hivyo  kumpa mtafiti laghba ya kulishughulikia. Data ya  makala hii  imekusanywa uwandani katika eneo la Kyamutwala  inakozungumzwa lahaja ya Kihamba. Kwa upande wa  Kyamutwala,  mtafiti amekusanya data katika kata za  Kamachumu, Ibuga, Muhutwe na Izigo. Katika eneo la Kiziba  data imekusanywa kutoka kata za  Buyango, Bugandika,  Ruzinga na Bwanjai inakozungumzwa lahaja ya Kiziba. Data hii  ya uwandani imepatikana kwa mbinu ya  ushuhudiaji, hojaji,  usaili na uchanganuzi wa matini za maktabani. Mtafiti  alishuhudia namna mbalimbali za kitahajia/hijai na  kimatamshi  kuhusiana na msamiati wa Kihaya katika lahaja ya Kihamba na  Kiziba. Aidha, data ilikusanywa kupitia hojaji ambapo  watafitiwa 80 waligawiwa dodoso na kuzijaza kikamilifu.  Kupitia mbinu ya usaili, mtafiti alifanya mahojiano ya ana kwa  ana na watafitiwa  wa makala hii na kuweza kubaini ulinganifu  na usiganifu uliopo baina ya msamiati wa lahaja  zinazoshughulikiwa katika  makala hii. Data ya maktabani  ilipatikana kwa mapitio ya matini mbalimbali zinazohusiana na  mada inayoshughulikiwa katika makala  hii. Utafiti huu  umeongozwa na Nadharia ya Umuundo iliyoasisiwa na  Ferdinand De Saussure. Matokeo ya utafiti huu yanaonesha  kwamba baadhi ya msamiati wa Kihamba na Kiziba hurandana  na baadhi husigana. Pia zimetolewa sababau za kufanana na  kutofautiana kwa msamiati wa lahaja hizo. Mtafiti wa makala  hii anapendekeza tafiti fuatizi zifafanue kwa kina sababu za  kutofautiana  na kufanana kwa msamiati wa lahaja hizi tofauti  na ilivyoelezewa katika makala hii kwani sababu ni nyingi.  Aidha, makala hii itatoa  hamasa kwa watafiti kufanya tafiti juu  ya lahaja za lugha mbalimbali. Vilevile, makala hii inatoa  mchango katika kukuza na kuendeleza  lugha za Kibantu na  taaluma ya isimu kwa ujumla. Pia itaongeza marejeleo faafu kwa  watafiti wa isimu. 


Journal Identifiers


eISSN: 2958-4914